Habari za Punde

KADA WA CCM PETER KAMFUMU AONGOZA KURA ZA MAONI UBUNGE IGUNGA

Rostam Aziz katika moja ya mikutano yake ya Chama siku za nyuma.
                                         ****************************************
KADA wa Chama Cha Mapinduzi  CCM, Peter Kamfumu, ameongoza kura za maoni zilizopigwa na Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM Wilaya ya Igunga Mkoani Tabora kwa ajili ya kuomba kugombea Ubunge Jimbo la Igunga lililoachwa wazi na aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, Rostam Azizi, aliyejiuzulu hivi karibuni.
Taarifa zilizopatikana kutoka mkoani Tabora zinaeleza kuwa, Kamfumu, ambaye pia ni Kamishna wa Nishati katika Wizara ya Nishati na Madini, amepata kura 588 kati ya kura 928 zilizopigwa na Wajumbe wa Mkutano huo katika uchaguzi uliofanyika jana Mjini Igunga.

Akizungumza na Sufianimafoto kwa njia ya simu, Katibu wa CCM Wilaya ya Igunga, Neema Adam, amesema kuwa katika kinyang'anyiro hicho walikuwa jumla ya wagombea 13 wanachama wa CCM  ambao wamepigiwa kura za maoni katika mkutano huo na hatimaye Kamfumu kuibuka kidedea kwa kuongoza katika kura hizo za maoni.

Aidha aliwataja Wanachama wengine waliopigiwa kura kuwa ni pamoja na Jafari Ali, aliyepata kura 163, Shamsi Feruzi, kura 36, Hamis Mapunda, kura 36,  Ngasa Nikolaus kura 18, Seif Hamis,  kura 13 na Shire Mashauri, kura 16.

Wengine ni Hamad Safari, kura 5, Mkoba Shaban, kura 5, Daniel Mboje, kura 4, Adam Kamani, kura 3 na Amina Fundikila, kura 7.

Aidha Katibu huyo wa CCM Wilaya ya Igunga alisema kuwa majina hayo yote yatapelekwa ngazi ya Mkoa ambayo nayo itayapitia na kisha kuyapeleka katika Kamati Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi kwa maamuzi zaidi.

No comments:

Post a Comment

SUFIANIMAFOTO Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.