Naibu Waziri wa Uchukuzi
na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (kulia) akizungumza na Meneja wa
Bandari za Ziwa Nyasa Bwana Ajuaye Msese wakisafiri kwa boti ndani ya ziwa hilo
kukagua upatikanaji wa huduma za mawasiliano na uchukuzi kwenye mwambao wa ziwa
hilo. Aliyevaa miwani ni Meneja Uendeshaji wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote
(UCSAF) Mhandisi Albert Richard
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akikagua upatikanaji wa huduma za mawasiliano na uchukuzi mkoani Rukwa katika ziara yake ya kikazi mkoani humo. Aliyeshika simu ni Mwenyekiti wa CCM mkoani humo Bwana Reina Lukala. KUSOMA ZAIDI BOFYA HAPA
Mkuu wa Wilaya ya Kalambo Mwalimu Julieth Binyula akimuonesha Meneja Uendeshaji wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) Mhandisi Albert Richard maeneo ambayo hayana mawasiliano wakiwa kwenye bandari ya Kasanga wilayani humo wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (hayupo pichani) ya kukagua upatikanaji wa huduma za mawasiliano na uchukuzi mkoani Rukwa
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (kushoto) akipata taarifa ya mkoa wa Rukwa kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa mkoa huo Mhe. Joachim L. Wangapo akiwa kwenye ziara ya kukagua upatikanaji wa huduma za mawasiliano na uchukuzi mkoani humo
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (kushoto) akisalimiana na Meneja wa Shirika la Simu Tanzania (TTCL) mkoa wa Rukwa Bwana Peter Kuguru alipowasili wakati wa ziara yake ya kukagua upatikanaji wa huduma za mawasiliano na uchukuzi mkoani humo
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (akiwa ndani ya gari la kwanza) akitoka kwenye bandari ya Kasanga iliyopo ziwa Tanganyika wakati wa ziara yake ya kukagua upatikanaji wa huduma za mawasiliano na uchukuzi mkoani Rukwa. Pembeni ni muonekano wa ziwa Tanganyika
*******************************************
Naibu Waziri wa Uchukuzi
na Mawasiliano wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta
Nditiye amefanya ziara ya kikazi ya kukagua upatikanaji wa huduma za
mawasiliano vijijini kwa wananchi waishio kwenye mwambao wa Ziwa Nyasa na
Tanganyika katika maeneo ya vijiji mbalimbali viliyopo kwenye mkoa wa Njombe,
Mbeya na Rukwa.
Mhandisi Nditiye
amefanya ziara hiyo ili kukagua upatikanaji wa huduma za mawasiliano kwa wananchi
waishio kwenye mwambao huo ili kujiridhisha kuhusu uwepo wa huduma hizo ambapo
Serikali kupitia Wizara hiyo inaipatia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF)
ruzuku inayoziwezesha kampuni za simu za mkononi kufikisha huduma za
mawasiliano vijijini na maeneo yasiyo na mvuto wa kibiashara.
Katika ziara hiyo,
Mhandisi Nditiye amebaini uwepo wa mawasiliano hafifu kwenye baadhi ya maeneo
na mahali pengine hamna mawasiliano yoyote kwa wananchi waishio mwambao wa ziwa
Nyasa na Tanganyika. “Nimesafiri kwa boti ndani ya ziwa Nyasa kutoka eneo la
Lupingu, Ludewa mkoani Nyasa hadi matema mkoani Mbeya na sasa kwenye bandari
hii ya Kabwe mkoani Rukwa, nimeshuhudia mwenyewe ukosefu wa mawasiliano ya
uhakika kwa wananchi waishio kwenye mwambao wa ziwa ambapo lolote likitokea
ukiwa ndani ya ziwa huwezi kabisa kuwasiliana,” amesema Mhandisi Nditiye.
Ameongeza kuwa Serikali
inatambua unuhimu wa wananchi kuwasiliana kwa kuwa mawasiliano yanachangia
ukuaji wa pato la wananchi na taifa kwa ujumla, yanawezesha na kurahisisha
shughuli za kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa eneo husika. Amesema kuwa
tayari Wizara kupitia UCSAF imefanya tathmini ya kufikisha huduma za mawasiliano
kwa kuzipatia ruzuku kampuni za simu za mkononi ili ziweze kujenga minara ya
simu za mkononi.
Mhandisi Nditiye amefafanua
kuwa ukosefu wa mawasiliano haimaanishi uwepo wa minara michache ya simu za
mkononi ya kampuni fulani na ukosefu wa mnara wa kampuni mojawapo ya
mawasiliano ya simu za mkononi, bali eneo ambapo hamna mnara wa simu za mkononi
wa kampuni yoyote ile.
Ameongeza kuwa hadi hivi
sasa Serikali imefikisha huduma za mawasiliano vijijini na maeneo yasiyo na
mvuto wa kibiashara kwenye maeneo mbalimbali nchini kwa kiwango cha asilimia
94, na ni maeneo machache tu ambayo yamebaki hayajafikiwa na huduma za mawasiliano.
“Serikali imejipanga na kuhakikisha kuwa huduma za mawasiliano zinawafikia
wananchi waliosalia ifikapo mwaka 2020 ambapo wananchi waishio kwenye mwambao
wa ziwa Nyasa na Tanganyika wamepewa kipaumbele hicho”, amesema Mhandisi
Nditiye.
Akitoa maelezo yake kwa
Mhandisi Nditiye kuhusu mpango huo wa Serikali wa kufikisha huduma za
mawasiliano kwa wananchi waishio kwenye mwambao, Meneja wa Uendeshaji wa UCSAF
Mhandisi Albert Richard amesema kuwa, tayari Mfuko umeyabaini maeneo hayo,
kufanya tathmini ya mahitaji ya minara na fedha husika ili kuweza kufikisha
huduma za mawasiliano kwenye baadhi ya maeneo ya wananchi waishio kwenye
mwambao wa maziwa hayo. “Tumetembea Ludewa kwenye Tarafa ya Mwambao yenye kata
nne za Kilondo, Lumbila, Lupingu na Makonde zilizopo mwambao wa ziwa Nyasa na
kubaini uwepo wa mawasiliano hafifu na mahali engine hakuna mawasiliano kabisa
ambapo Serikali imetenga kiasi cha dola za marekani 252,500 ambazo zitatumika
kufikisha mawasiliano”. Amesema Mhandisi Richard.
Akizungumza na Mhandisi Nditiye kuhusu hali ya
mawasiliano na miundombinu mengine kwenye mkoa huo, Mkuu wa Wilaya ya Ludewa
Mhe. Andrea Tsere amesema kuwa tayari Serikali kupitia Wakala wa Barabara
Vijijini (TARURA) inaendelea na kazi ya kupita kwenye eneo la mwambao wa ziwa
Nyasa ili kuweza kujenga barabara kwa kuwa wananchi waishio eneo hili hawana
barabara ya uhakika. Pia, amemshukuru Mhandisi Nditiye kwa kufanya ziara hiyo
na kuzungumza na wananchi ambapo amewahakikishia kuwa Serikali inakamilisha
ujenzi wa meli mpya kwa ajili ya eneo hilo na itajenga minara ya mawasiliano
ili kutimiza ahadi ya Serikali ya Awamu ya Tano inaayoongozwa na Dkt. John
Pombe Magufuli ya kuwatumikia wananchi.
Katika hatua nyingine,
Mhandisi Nditiye akiwa mkoani Rukwa kwenye bandari ya Kabwe na Kasanga na
bandari ya Itungi, iliyopo Kyela mkoani Mbeya, amelielekeza Shirika la Simu
Tanzania (TTCL) kushirikiana na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari kufunga mitambo
ya mawasiliano kwenye meli mpya ili abiria waweze kuwasiliana wakiwa ndani ya
meli kwa kuwa wengine ni wafanyabiashara wanaosafirisha mizigo ndani na nje ya
nchi kupitia maziwa hayo. Naye Katibu Tawala wa Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya
Bwana Godfrey Kawache amemueleza Mhandisi Nditiye kuwa kuna ukosefu wa
mawasiliano kwenye baadhi ya maeneo ya kata ya Nguna, Ngonga, Busele,
Kajungumele na maeneo ya Kandete na Ibada.
Mhandisi Nditiye
aliambatana na Mkuu wa Wilaya ya Kalambo Mwalimu Julieth Binyula na wa Nkasi Bwana Said Mohamed Mtanda wa Mkoa
wa Rukwa akiwa katika ziara yake ya kukagua upatikanaji wa huduma za
mawasiliano na uchukuzi katika maeneo ya mkoani Rukwa. Bwana Mtanda amemuomba
Mhandisi Nditiye kuwaelekeza wataalamu wake kushirikiana na Ofisi za Wakuu wa
Wilaya kutekeleza majukumu ya Serikali kwa manufaa ya wananchi.
No comments:
Post a Comment