Habari za Punde

ANGA LA TANZANIA RASMI KUTUMIKA-WAZIRI MHANDISI KAMWELWE

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe, akifafanua jambo kwa Waandishi wa Habari (hawapo pichani), alipokutana nao kutoa taarifa ya kuruhusu anga la Tanzania kutumika kwa ndege za abiria, biashara na mizigo, jijini Dodoma leo. 
Mkurugenzi wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Hamza Johari (kushoto) na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini, Mhandisi Julius Ndyamukana (kulia), wakimsikiliza Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe (hayupo pichani), jijini Dodoma leo wakati alipokutakana na waandishi wa habari kuruhusu anga la Tanzania kutumika kwa ndege za abiria, biashara na mizigo.
********************************************

Serikali ya Tanzania imefuta rasmi zuio la safari za ndege baada ya taathimini ya mambukizi ya COVID -19 iliyofanywa nchini kubaini kupungua kwa maambukizi na idadi ya wagonjwa na kurejesha huduma za usafiri kama ilivyokuwa awali.
Akifuta zuio hilo jijini Dodoma leo Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe ameziagiza Mamlaka ya Usafiri wa Anga Nchini (TCAA), Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA), Kampuni ya  Kusimamia na kuendeleza Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KADCO) na Kampuni ya Ndege Nchini (ATCL) kuanza kutoa huduma bila kikwazo na kuzingatia taratibu za kiafya zilizotolewa na Shirika la Afya Ulimwenguni na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Nchini.
“Kupitia Tangazo hili natamka kuwa ndege zote za kibiashara, misaada, kidiplomasia, dharura na ndege maalum zinaruhusiwa kuruka na kutua katika viwanja vyetu nchini kama ilivyokuwa awali” Amesema Waziri Mhandisi Kamwelwe.
Waziri Mhandisi Kamwelwe amezitaka Taasisi hizo kuhakikisha abiria wote wanaoingia nchini wanapimwa joto ili kuendelea kujikinga na maambukizi yanayoweza kutokea kutokana na muingiliano wa watu. 
Waziri Mhandisi Kamwelwe ameongeza kuwa kufunguliwa kwa anga hilo kutarejesha fursa za kibiashara hasa katika eneo la utalii na kuinua pato la Taifa. 
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilitoa tamko la kufunga rasmi  ndege za abiria za mashirika ya ndege ya kimataifa kuingia nchini Mei 2020 baada ya kujiridhisha kuwepo na ongezeko la kuenea kwa Virusi vya Korona
Katika hatua nyingine Waziri Mhandisi Kamwelwe amesema kwa upande wa Usafiri wa Malori kati ya Tanzania na Rwanda Serikali za nchi hizo zimekubaliana masharti nane ili kuendelea kudhibiti kuenea kwa virusi kati ya nchi hizo mbili. 
Waziri Mhandisi Kamwelwe amesema pamoja na mambo mengine Serikali hizo zimekubaliana mizigo inayoelekea Rwanda kushuhushwa katika vituo maalum ikiwemo Rusumo na Kagitumba isipokuwa mzigo wa mafuta, Magari yanayokwenda Nchini Demokrasia ya Kongo (DRC) kupitia Rwanda itasindikizwa bure hadi kwenye mpaka wa Rwanda na DRC.
Magari ya mizigo yataruhusiwa kusafiri kuanzia sa 12.00 asubuhi hadi 12.00 jioni, kuboresha taratibu za upakiajia na upakuaji wa mizigo katika mipaka, kupunguza vituo vya kusimama.
Waziri Mhandisi Kamwelwe ameongeza kuwa madereva wote wanaosafirisha mizigo watapimwa mwanzoni mwa safari na kwenye mipakani baada ya kuwasili.
Aidha, amewataka wadau wote wa usafirishaji kuhakikisha changamoto zote zinazowakabili ziwasilishwa Wizarani ili kufanyiwa kazi kabla ya kuathiri biashara katika mipaka yote nchini.

No comments:

Post a Comment

SUFIANIMAFOTO Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.