Habari za Punde

*BALOZI SEIF AZINDUA MRADI WA MAJI SAFI SKULI YA CHOKOCHO, PEMBA

 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi, akiangalia maji katika kisima cha maji kiliopo Skuli ya Chokocho mara baada ya kuuzindua mradi wa maji safi na salama wa Michenzani hadi chokocho.
 Waziri wa Sayansi na Teknolojia Wa Serikali ya Muungano Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, ambaye ni muanzilishi wa mradi huo akitoa maelezo mbele ya Mgeni rasmi Balozi Seif na kuchangia mipira na mabomba ya maji kusambazia maji katika Jimbo la Mkanyageni.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi, akimkabidhi Katibu wa Kamati ya Maendeleo ya Jimbo la Mkanyageni, Ame Vuaa Shein, mipira na Mabomba ya kusambazia maji katika mradi uliozinduliwa rasmi na Balozi Seif.
******************************
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema ili huduma za maji safi na salama  ziendelee kudumu kizazi cha sasa kinapaswa kuzingatia utunzaji wa mazingira samba na kuheshimu miundo mbinu ili sekta hiyo itowe huduma kiuhakika.
Balozi Seif alieleza hayo wakati akizindua mradi wa Maji safi  na salama wa Michenzani hadi chokocho uliojumuisha visiwa vidogo vidogo vya vilivyomo pembezoni mwa Jimbo la Mkanyageni Wilaya ya Mkoani Mkoa wa Kusini Pemba.
Uzinduzi huo unaotarajiwa kuhudumia zaidi ya wakazi wa 21,841 wa Vijiji vya Mkanyageni, Chokocho,Michenzani, Kisiwa Panza na Makoongwe ni miongoni mwa shamra shamra za maadhimisho ya kutimia miaka 49 ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964.
Balozi Seif alisema wakati umefika kwa Wananchi kushirikiana na Serikali sambamba na Viongozi wao wa jimbo kuendesha kampeni ya upandaji miti ili rasilmaliya maji  iliyobarikiwa nchi iweze kudumu kwa muda mrefu.
“ Hii tabia iliyozoeleka hapa kwetu ya mtu kukuta mfenesi twende, muembe twende, au mti wowote twende kwa ushawishi wa msumeno wa Moto kwa kweli imetufikisha pabaya na tunapaswa kuwa na tahadhari na tabia hii mbaya”. Alifafanua Balozi Seif.
Alifahamisha kwamba licha ya juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali za kumarisha huduma za maji lakini bado sekta  hii inaonekana kuharibiwa kwa makusudi na baadhi ya watu na isipodhibitiwa upungufu wa huduma hii utegemewe kuongezeka.
Balozi Seif aliwaasa wabunge na wawakilishi kuwa waangalifu katika kutambua mahitaji ya wananachi wanaowaongoza katika suala zima la kuimarisha miradi ya kiuchumi na maendeleo.
Usimamizi wa maendeleo ya Jimbo umo ndani ya usimamizi wa wabunge na wawakilishi ambao ndio waliokubali kubeba jukumu hilo muhimu la kuwatumikia.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimshukuru na kumpongeza Waziri wa Sayansi na Teknolojia wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Profesa Makame Mnyaa Mbarawa ambaye ni mzaliwa na Jimbo la Mkanyageni Pemba  kwa juhudi zake za kupigania maendeleo ya jimbo hilo.
Balozi Seif alisema kitendo cha Profesa Mbarawa cha kutekeleza ahadi alizotowa wakati wa kampeni za uchaguzi za mwaka 2010 licha ya kukosa fursa ya kuliongoza jimbo hilo katika wadhifa wa Mbunge lakini alionyesha ushujaa kwa kukamilisha ahadi hizo.
“ Profesa Makame Mnyaa Mbarawa anafaa kupongezwa na jamii yote kwa uungwana wake wa kutekeleza ahadi alizotoa wakati wa kampeni licha ya kukosa fursa aliyoiomba ya kuwatumikia wananchi wa Jimbo la Mkanyageni”. Alionyesha furaha yake Balozi Seif.
Aidha aliwaeleza wananchi hao wa Jimbo la Mkanyageni kwamba Serikali kupitia mamlaka ya Maji { ZAWA } imeshasambaza huduma za Maji safi na salama kwa zaidi ya asilimia 89%.
Aliipongeza mamlaka ya maji kwa jitihada zake za kusambaza huduma ya maji mjini na vijijini.
Mapema Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Madini Nd. Mustafa Aboud Jumbe alisema lengo la Serikali kupitia Wizara hiyo ni kuwaondoshea kero ya Wananchi ili wapate fursa ya kushiriki vyema katika harakati za Maendeleo.
Nd. Mustafa alisema mradi wa maji safi na salama wa Michenzani hadi Chokocho ambao ni miongoni mwa juhudi hizo itasaidia kuwaondoshea wakaazi wa maeneo hayo wapatao 21,841.
Alisema mradi huo ulioanza harakati za matengenezo mwezi Julai mwaka 2011 na kumalizika mwezi Septemba mwaka 2012 umehusisha Visima Viwili vitakavyosambaza maji katika Vituo viwili vikubwa katika eneo hilo.
Akitoa shukrani zake Waziri wa Sayansi na Teknolojia wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Profesa Makame Mnyaa Mbarawa alisema chimbuko la mradi huo lilianza wakati wa kampeni za uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.
Aliwaasa Wananachi wa Jimbo hilo kuacha kubeza maendeleo wanayopelekewa ambayo mengine ni ahadi zilizotolewa ambazo hazina budi kutekelezwa na wale walioshiba uungwana.
Mradi wa Maji safi na salama wa Michenzani hadi Chokocho umegharimu jumla ya shilingi za Kitanzania Milioni 120,535,224/- ambazo kati ya hizo Profesa Makame Mnyaa Mbarawa ametoa shilingi Milioni 73,000,000/-
Profesa Mbarawa pia akakabidhi mabomba na Mipira ya maji ili kusambazia maji katika vijiji hivyo vikiwa na thamani ya shilingi Milioni 23,000,000/-.
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
7/1/2013.

No comments:

Post a Comment

SUFIANIMAFOTO Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.