Rais Dkt. Jakaya Kikwete (kushoto) akipokea hati ya utambulisho kutoka kwa Balozi mpya kutoka nchini Italia Dkt. Luigi Scotto, wakati wa hafla fupi iliyofanyika Ikulu- Dar es Salaam, leo mchana.
Balozi mpya anayewakilisha nchi ya Italia nchini Tanzania Dkt, Luigi Scotto (katikati waliovaa suti) pamoja na maafisa wakuu wa Itifaki wakiwa katika wimbo wa taifa.leo katika hafla hiyo ya utambulisho Ikulu Dar es Salaam.
Bolozi mpya wa Italia nchini Tanzania Mh. Dkt, Luigi Scotto (kulia) akisalimiana na baadhi ya maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje, leo katika hafla hiyo Ikulu jijini Dar es Salaam. Picha na Mwanakombo Jumaa-MAELEZO.
********************************
NA ELEUTERI MANGI –MAELEZO
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amepokea hati za utambulisho za Balozi mpya wa Italia katika Tanzania Dkt. Luigi Scotto.
Mapokezi hayo yalifanyika katika halfa fupi iliyofanyika Ikulu leo jijini Dar es Salaam.
Rais Kikwete amemtaka Balozi huyo mpya kuisaidia kuyashawishi makampuni zaidi ya Italia kuja kuwekeza na kuboresha mahusiano ya kiuchumi wa baina ya nchi hizo mbili.
“Tumekuwa na makampuni makubwa ya Italia yaliyopata kuwekeza katika uchumi wa Tanzania ikiwa ni pamoja na Agip na Incar lakini bado tunahitaji uwekezaji zaidi ili tuweze kuimarisha zaidi uchumi wetu,” Rais Kikwete alimwambia Dkt. Scotto.
Aidha, Rais Kikwete ameishukuru Italia kwa misaada ambayo nchi hiyo imekuwa inatoa kuchangia maendeleo ya Tanzania ikiwamo kugharimia ujenzi wa Barabara ya Dar es Salaam Bagamoyo.
Naye Balozi huyo mpya kwa upande wake amesema kuwa amefurahi kuteuliwa kuwa Balozi katika Tanzania.
“Ndoto yangu kubwa tokea nikiwa mtoto ilikuwa ni kufanya kazi katika nchi iliyomtoa Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere” alisema Balozi Scotto.
Balozi huyo alipowasili katika viwaja vya Ikulu alipokewa na wenyeji wake na nyimbo za mataifa hayo ziliimbwa zikiongozwa na bendi maalumu iliyoandaliwa kwa ajili ya mapokezi ya balozi.
Balozi Dkt. Scotto anachukua nafasi ya mtangulizi wake nchini Perluigi Velardi aliyemaliza muda wake wa kulitumikia taifa lake nchini.
No comments:
Post a Comment