Habari za Punde

BENKI YA NMB YAZIDI KUWANUFAISHA MADEREVA WA BODABODA

 Meneja Mahusiano wa Idara ya Kadi, Benki ya NMB, Yusuph Achayo, akimpongeza dereva wa Boda boda, Baraka Ally, aliyezawadiwa zawadi ya simu mpya aina ya Tecno Pop 2 baada ya kufanya miamala zaidi ya 200 ya kibenki kwa mwezi, wakati wa hafla fupi ya kukabidhi zawadi za simu kwa 
washindi iliyofanyika Makao Makuu ya benki hiyo, jijini Dar es Salaam, leo. Katikati ni Meneja Mwandamizi wa Idara ya Kadi, Manfredy Kayala.
Meneja Mahusiano wa Idara ya Kadi, Benki ya NMB, Yusuph Achayo, akimpongeza dereva wa Boda boda, Baraka Ally, aliyezawadiwa zawadi ya simu mpya aina ya Tecno Pop 2 baada ya kufanya miamala zaidi ya 200 ya kibenki kwa mwezi, wakati wa hafla fupi ya kukabidhi zawadi za simu kwa washindi iliyofanyika Makao Makuu ya benki hiyo, jijini Dar es Salaam, leo. Katikati ni Meneja Mwandamizi wa Idara ya Kadi, Manfredy Kayala.(Picha na Muhidin Sufiani).
***********************************************
Na Mafoto Reporter
MWENYEKITI wa Chama cha Madereva na Wamiliki wa Bodaboda Mkoa wa Dar es Salaam (CMPD), Michael Masawe, ameitaja Kampeni ya NMB MastaBODA, inayolenga kuirasimisha sekta ya usafirishaji kwa njia ya pikipiki, kuwa mkombozi wa vijana katika mkoa wake na taifa kwa ujumla.
Masawe aliyasema hayo leo wakati wa hafla ya kukabidhiwa zawadi za simu janja ‘smartphone’ kwa madereva wanane wa pikipiki, ambao ni sehemu ya madereva 68 wa huduma hiyo maarufu kama bodaboda, waliotangazwa washindi wa pesa taslimu na simu janja.
NMB MastaBoda, inayoratibiwa na Benki ya NMB na Kampuni ya Mastercard QR, ilianzishwa Oktoba 16 na kutarajia kufikiwa ukomo mwishoni mwa Januari mwakani, ambako madereva watakaofanya miamala mingi kupitia Mastercard QR, watajipatia pikipiki aina ya Boxer.
Akizungumza katika hafla ya kukabidhi zawadi za simu janja aina ya Tecno Pop 2F na kofia ngumu za madereva pikipiki ‘Helmet,’ Masawe alisema katika kipindi cha miezi miwili ya uwepo wa NMB MastaBODA, maisha ya wengi miongoni mwa wanachama wake yamebadilika.
Alifafanua kuwa, MastaBODA imesaidia kujenga heshima miongoni mwa madereva wa huduma hiyo, ambao sio tu wamepanua wigo wa kujitunzia akiba kupitia mfumo rasmi wa Mastercard QR, bali pia kujiwezesha kushinda zawadi mbalimbali kulingana na uwingi wa miamala yao kwa wiki na mwezi.
Katika hafla hiyo, iliyofanyika Makao Makuu ya NMB jijini Dar es Salaam, madereva bodaboda nane, walijinyakulia simu hizo, hivyo kufanya idadi ya walionufaika na huduma hiyo kufikia 60, kwani kabla ya jana, madereva 60 walijishindia pesa taslimu kiasi cha Sh. 50,000 kila mmoja.
Madereva waliojinyakulia simu janja jana na vituo vyao vya kazi kwenye mabano ni; John Haonga (Mabibo), Abdallah Mohamed (Morocco), Florian Celestine, Twalha Mfinanga na Mohamed Abdallah (Buguruni Rozana), Ebenezer Elisha (Mwenge), Ladislaus Laiza (Ubungo Plaza) na Adam Gunza (Mlimani UDSM).
 Meneja Mwandamizi wa Idara ya Kadi Benki ya NMB, Manfredy Kayala, akimkabidhi zawadi ya simu mpya aina ya Tecno Pop 2 dereva wa Bodaboda kituo cha Buguruni Rozana, Mohamed  Abdallah, baada ya kuibuka mshindi wa kufanya mialama ya kibenki zaidi ya 200 kwa mwezi kulipwa nauli na abiria wake kwa kutumia huduma mpya ya Master Boda QR, wakati wa hafla fupi ya kukabidhi zawadi za washindi iliyofanyika Makao Makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam, Kulia ni Meneja Mwandamizi wa Idara ya Bidhaa za Kadi, Lupia Matta na Mwenyekiti wa Chama cha Waendesha Bodaboda na Bajaji Mkoa wa Dar es Salaam, Michael Massawe.
  Meneja Mwandamizi wa Idara ya Kadi Benki ya NMB, Manfredy Kayala, akimkabidhi zawadi ya simu mpya aina ya Tecno Pop 2 dereva wa Bodaboda kituo cha Mwenge, Ebenezer Elisha, baada ya kuibuka mshindi wa kufanya mialama ya kibenki zaidi ya 200 kwa mwezi kulipwa nauli na abiria wake kwa kutumia huduma mpya ya Master Boda QR, wakati wa hafla fupi ya kukabidhi zawadi za washindi iliyofanyika Makao Makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam, Kulia ni Meneja Mwandamizi wa Idara ya Bidhaa za Kadi, Lupia Matta na Mwenyekiti wa Chama cha Waendesha Bodaboda na Bajaji Mkoa wa Dar es Salaam, Michael Massawe.
 Dereva wa Bodaboda wa Kituo Sayansi Adam, akiibusu simu yake mpya aina ya Tecno Pop 2 aliyokabidhiwa baada ya kuibuka mshindi wa kutumia huduma mpya ya Master Boda QR kwa 
kufanya miamala zaidi ya 200 kwa mwezi kulipwa nauli na mteja wake kwa kutumia Master Boda QR, wakati wa hafla ya kukabidhi zawadi za washindi iliyofanyika Makao Makuu ya NMB jijini 
Dar es Salaam.
 Viongozi wa NMB wakiwa katika picha ya pamoja na washindi wa simu mpya baada ya kukabidhiwa katika Makao Makuu ya Benki hiyo jijini Dar es Salaam. Washindi hao wameshinda baada ya kufanya miamala ya kibenki zaidi ya 200 kwa mwezi kulipwa nauli na abiria wao kwa kupitia huduma mpya ya Master Boda QR. 
 Meneja Mahusiano wa Idara ya Kadi, Benki ya NMB, Yusuph Achayo,  akiwa katika picha ya pamoja na washindi.
Kwa upande wake, Meneja Mwandamizi Kitengo cha Bidhaa za Kadi wa NMB, Rupia Mashauri, alisema mwitikio wa vijana katika kuchangamkia fursa zinazoambana na huduma ya MastaBODA ni mkubwa na kwamba wamejipanga kuwafikia wengi zaidi kuanzia Januari mwakani.
Mashauri alisema kuwa, kuelekea kuhitimisha kampeni hiyo mwishoni mwa mwezi ujao, NMB na Mastercard QR wamejizatiti kuwafikia madereva bodaboda wapatao 75,000 kati ya milioni 2 wanaotoa huduma hiyo kote nchini, ili kuwaunganisha na mfumo huo wa utoaji huduma kisasa.
Aliwataka madereva bodaboda kuhakikisha wanajituma ili kuongeza miamala yao kwa siku, wiki na mwezi, ili kunufaika na zawadi mbalimbali, ili pia kujiwekea nafasi kubwa ya kupata mikopo ya pikipiki na bajaji zinazotarajiwa kutolewa chini ya huduma hiyo kuanzia Januari mwakani.
Wakitoa neno la shukrani, washindi hao waliipongeza NMB kwa wazo lililozaa huduma ya NMB MastaBODA na kwamba kupitia huduma hiyo, wameweza kujiwekea akiba pamoja na kuepuka matumizi yasiyo ya lazima, sambamba na kumaliza tatizo la upotevu wa pesa zao nyakati za ajali.

No comments:

Post a Comment

SUFIANIMAFOTO Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.