Habari za Punde

NEC YATEUA WAGOMBEA 77 KUTOKA VYAMA 17 KUGOMBEA UDIWANI KATIKA KATA 14

Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Kilosa, Kisena Magena Mabuba (kushoto) akimsaidia Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi ngazi ya Kata ya Magubike, Juma Hamis Ngwele kubadika fomu za uteuzi za wagombea udiwani katika Kata ya Magubike katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa.
Wagombea sita wameteuliwa kuwa wagombea wa udiwani kwenye uchaguzi mdogo wa Kata ya Magubike. Wagombea hao na vyama vyao kwenye mabano ni pamoja na Godfrey Pascal Musa (CCK),  Zinduna Omary Said (UPDP), Abuu Mjema Msofe (CCM), Ten Edna Atanas (AAFP), Mariam Said Ndombere (CUF) na  Esta Hosea Makono (ADC).
Wagombea na wananchi wa Kata ya Magubike wakikagua fomu za uteuzi za wagombea walioteuliwa kugombea udiwani katika Kata hiyo. 
**********
Na Mwandishi Maalum-NEC
WAGOMBEA 77 kutoka vyama 14 vyenye usajili wa kudumu wameteuliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuwania nafasi wazi za udiwani katika Kata 14 za Tanzania Bara ambazo zinataraji kufanya uchaguzi mdogo  Julai 13,2023.

Tume ya Taifa ya Uchaguzi imetangaza tarehe 13 Julai, 2023 kuwa siku ya uchaguzi mdogo wa madiwani katika kata 14 za Tanzania Bara ambapo uteuzi wa wagombea kwa ajili ya uchaguzi huo umefanyika jana tarehe 30 Juni, 2023.
 
Awali Fomu za uteuzi wa wagombea hao zilianza kutolewa kuanzia tarehe 24 Juni, 2023 hadi tarehe 30 Juni, 2023 na jumla ya wagombea 90 walichukua fomu za uteuzi.
 
Kati ya wagombea hao 90 waliochukua fomu, wanaume walikuwa 74 na wanawake walikuwa 16 lakini hadi dirisha la uteuzi linafungwa saa 10 kamili jioni jana ni jumla ya wagombea 77 waliteuliwa kati ya hao wanaume ni 63 na  wanawake ni 14. Aidha, jumla ya wagombea 13 hawakurejesha fomu za uteuzi.
 
Aidha, Katika kata 13 wameteuliwa wagombea zaidi ya mmoja, huku Kata moja ya Mnavira iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Masasi mgombea mmoja tu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) ameteuliwa kutokana na wagombea wa vyama vingine kutorejesha fomu za uteuzi.
 
Wagombea walioteuliwa wanatoka katika vyama vya siasa 17 ambavyo ni AAFP, ACT – WAZALENDO, ADA – TADEA, ADC, CCK, CCM, CUF, DEMOKRASIA MAKINI, DP, NCCR – MAGEUZI, NLD, NRA, SAU, TLP, UDP, UMD na UPDP. 
Kwa mujibu wa sharia Ilipofika saa 10:00 Jioni wasimamizi wa uchaguzi walibandika fomu za uteuzi za wagombea walioteuliwa katika eneo la wazi ili watu wanaoruhusiwa kisheria waweze kuweka pingamizi, fomu hizo zitaendelea kubandikwa hadi saa 10:00 jioni leo siku ya tarehe 01 Julai, 2023. Hadi sasa hakuna pingamizi lolote lililopokelewa na wasimamizi wa uchaguzi katika kata zote 14. 
Kata zinazotarajiwa kufanya uchaguzi mdogo ni pamoja na Ngoywa iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge, Kalola iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Uyui, Sindeni iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, Potwe iliyopo Halmashauri ya Muheza, Kwashemshi iliyopo Halamshauri ya Wilaya ya Korogwe, Bosha iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga, Mahege iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti na Bunamhala iliyopo katika Halmashauri ya Mji wa Bariadi. 
Nyingine ni, Njoro na Kalemawe zilizopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Same, Mnavira iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Masasi, Kinyika iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Makete, Magubike iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa na Mbede iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe. 
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kampeni kwa ajili ya Uchaguzi Mdogo kwenye kata hiyo zitaanza leo tarehe 01 hadi 12 Julai, 2023 na uchaguzi utafanyika tarehe 13 Julai, 2023.
Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi Bi Kurwa Izack wa Kata ya Bosha iliyopo Halmashauri ya Mkinga mkoani Tanga  akibandika fomu za uteuzi katika eneo la wazi kuonyesha wagombea ambao  wameteuliwa kuwania udiwani wa kata hiyo. Wagombea walioteuliwa na vyama vyao kwenye mabano ni Zakaria Samwel Laizer  (ACT – WAZALENDO, Simon Chaless Kayanda (ADC), Mashaka Hauseni Mgungu (CCM), Omary Mbaruku Bendera  (CUF) na William Julius Pasikali (DP).
Wananchi wa Kata ya Bosha wakipiga picha fomu za uteuzi.
Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi wa Kata ya Kalemawe katika Halmashauri ya Same, Christopher Mteri akibandika fomu za uteuzi ambapo wagombea watatu wameteuliwa kugombea udiwani katika kata hiyo. Walioteuliwa ni Jofrey Mtwa Jofrey (CCM), Musa Hendrish Filipo (CUF) na Helena Juma Kigono (TLP). 
Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi Kata ya Kalola katika Halmashauri ya wilaya ya Uyui mkoani Tabora, Marco Mande Ezekiel akibandika fomu ya uteuzi mara baada ya kumalizika kwa zoezi za uteuzi wa wagombea wa nafasi ya udiwani katika kata ya Kalola  jana Juni 30, 2023. 
Wagombea wa Udiwani walioteuliwa na vyama vyao katika mabano ni Issa John Walter- (NRA), Abdalah Silvery Koni (CCM), Alexander Ndoya Mpalaza (NLD), Haji Omary Tetema (CUF), Baraka Wandambwe Kalonga (CCK), Jeronimus Francis Bonifas (DP), Timoth Sitivia Nkwabi (AAFP), Yasin Juma Masilamba (ADC) na  Khadija Juma Iddi (NCCR – Mageuzi).
Baadhi ya wagombea walioteuliwa kugombea udiwani katika kata ya Kalola halmashauri ya wilaya ya Uyui mkoani Tabora wakiangalia fomu za Uteuzi mara baada ya kubandikwa nje ya ofisi ya msimamizi msaidizi wa uchaguzi leo tarehe 30 Juni, 2023.
Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Kibiti, Hemed Said Magari akibandika fomu za uteuzi wa Wagombea Udiwani Kata ya Mahege, Halmashauri ya Kibiti Mkoani Pwani. Jumla ya Wagombea sita kati ya saba waliochukua fomu wameteuliwa kugombea nafasi hiyo ya udiwani unaotarajiwa kufanyika tarehe 13 Julai, 2023. Wagombea wa Udiwani walioteuliwa na vyama vyao katika mabano ni Hamada Juma Hingi (CCM), Mrisho Miraji Jongo  (CUF), Sultani Saidi Mpondi (UPDP), Seif Adam Mkokwa (UMD), Mussa Juma Muramuah (UDP), Athumani Sadiki Mzuzuri (NRA) Na Mussa Sultani Mussa (ADC).
Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi wa Kata ya Mnavira iliyopo katika Halmashauri ya Masasi, Stella Stuart akibandika fomu ya uteuzi ya Mgombea wa udiwani aliyeteuliwa. Katika Kata hiyo Mgombea mmoja alirejesha fomu na Tume kumteua Nyasa Bakari Seifu wa CCM kuwa mgombea pekee.
Nyasa Bakari Seifu wa CCM akikagua fomu zake baada ya kubandikwa katika ubao wa matangazo.
Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi Kata ya Bunamhala katika Halmashauri ya Mji wa Bariadi ,Mkoani Simiyu ndg Kalimbiya  Kiyumbi Gambuna  akibandika Fomu za Uteuzi za wagombea walioteuliwa kugombea kiti cja Udiwani katika kata hiyo kwaajili ya Uchaguzi mdogo kwa kata 14 za Tanzania Bara,unaotaraji kufanyika Julai 13 mwaka huu.
Wagombea walio teuliwa na vyama vyao katika mabano ni Hamidu Mohamed Juma (SAU),Malimi Sayi Migwata(NLD),Tilusubya Mugana Mwangwa(NRA), Marugu Petro Ngasa(DP), Iddy Mtaka Shabani (UMD), Roberti Mashaka Igonji(UPDP), Paulo Shija Masanja(TADEA), Nkamba Rehema Zabron (CCM), Zainabu Bahame(AAFP), Joyce Zacharia(NCCR MAGEUZI), John Mageta Sweya (UDP), Tilu Andrea Ifunya (DEMOKRASIA MAKINI), Mboje Nilla Makula(ADC) na Hamza Shaban Masharo(CUF)
Wagombea na wananchi wakiangalia fomu zilizowekwa wazi Kata ya Bunamhala.
Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi Kata ya Ngoywa Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge Mkoa wa Tabora, Boniface Charles akibandika fomu za uteuzi baada ya zoezi la uteuzi kukamilika. Wagombea walio teuliwa na vyama vyao katika mabano ni Revocatus Evaristi Mkama (AAFP), Ramadhani Abdalla Maselele (ACT – WAZALENDO), Abdul Jumanne Furutuni (ADA – TADEA), Leonard Mwagala Kwilasa (CCM), Abdallah Ibrahim Katala (CUF) na  Manengelo Kija Magadula (UDP).
Wagombea wa Kata ya Ngoywa wakiangalia fomu baada ya uteuzi na kubandikwa.
Msimamizi Msaidizi wa  Uchaguzi Kata ya Njoro katika Halmashauri ya Wilaya   ya Same, Benedict Lopa  akibandika fomu za uteuzi za wagombea udiwani wa Kata hiyo. Walioteuliwa ni Kassimu Rashidi Msuya (ADC), Omari Abeid Abdala (CCM), Rafael Mbonea Mrutu (NCCR – Mageuzi) na Paulo Juma Mshana (TLP). 
Mmoja wa wagombea akiangalia fomu za uteuzi baada ya kuwekwa wazi na Msimmizi Msaidizi wa Uchaguzi ngazi ya Kata katika kata ya Potwe katika Halmashauri ya Muheza,  Kassim. A. Muhando. Wagombea walioteuliwa  na vyama vyao kwenye mabano ni pamoja na Keneth Matias Libangile (NCCR Mageuzi),Yusha Twaha Said (Demokrasia Makini), Othman Juma Bahari (CCM), Denis Josep Semzungu (ADC) Juma Peter Nind (CUF) na Amir Bakari Kidungwe (SAU).
Wagombea wa Udiwani wa Kata ya Mbede wakiwa pamoja na wanachama wao wakishuhudia fomu za uteuzi katika mbao za matangazo za Kata hiyo baada ya zoezi la uteuzi kukamilika. Wagombea wawili Vicent Benard  Mauga (CCM) na Rebeca Gaspa Kambenga (UDP) waliteuliwa kuwania nafasi hiyo.
wagombea na wananchi wa Kata ya Sindeni, wakiangalia fomu za uteuzi zilizobandikwa na Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi ngazi ya Kata, Simon Challe ambapo watu nane wameteuliwa kuwa wagombea wa udiwani kwenye uchaguzi mdogo wa Kata ya Sindeni iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Handeni. Wagombea hao ni Athumani Mgaza (CUF), Mary Moses (UPDP), Mwajuma Mirambo (UMD), Emiliana Hudson (CCK), Hemedi Kilongola (CCM), Hadija Kawaga (ADC), Saidi Mgandi (UDP) na Sadiki Mbelwa (NCCR MAGEUZI).

No comments:

Post a Comment

SUFIANIMAFOTO Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.