Habari za Punde

*ALLY CHOKI, SUPER NYAMWELA WATIMKIA JAPAN KUONGEZA MAKALI, BENDI YAFUNGWA

Na Ripota wa Sufianimafoto, Dar
MKURUGENZI wa bendi ya Extra Bongo 'Wazee wa Kizigo', Ally Choki na Kiongozi wa Shoo wa bendi hiyo, Super Nyamwela, wameondoka nchini wiki iliyopita kuelekea nchini Japan kwa ajili ya kufanya maonesho kadhaa binafsi nje ya bendi hiyo.

Akizungumza na Mtandao huu, kabla ya kuondoka nchini Ally Choki, alisema kuwa wamepata mwaliko kama watu binafsi na si kundi zima, jambo ambalo limewalazimu kusitisha maonyesho yao ya kawaida hapa nchini kwa muda ili kukamilisha safari hiyo inayotarajia kuwa ni zaidi ya miezi mitatu.

Nyamwela akipozi huko umangani.
Wakiwa nchini Japan, wanatarajia kufanya maonyesho kadhaa waliyoandaliwa na mwenyeji wao, wakiwa na bendi iliyoandaliwa kufanya nao mazoezi maalum kwa ajili ya shoo hizo, ambapo pia wanatarajia kufanya shoo na mwanamuziki mahiri wa siku nyingi anayepiga kazi zake nchini humo, Fresh Jumbe. 

Aidha Choki alisema kuwa kwa kipindi chote watakachokuwa nje ya Nchi Wanamuziki wa bendi yake watakuwa likizo kutokana na mashabiki walio wengi wa muziki wa dansi kutoamini bendi bila kiongozi au Staa wanayempenda kuwepo.

''Naogopa kuwaachia bendi wanamuziki wangu yasije yakawakuta yale yaliowahi kuwakuta wanamuziki wa Christian Bella, huko Kimara ambapo walizua mtafaruku mkubwa baada ya kutaka kupiga shoo bila kuwepo Bella huku mmoja akivaa Pama na kujifanya ni Bella na aliposhitukiwa alivuliwa pama na kushambuliwa na mashabiki jambo lililozua mtafaruku mkubwa na kusababisha kuvunjika kwa baadhi ya vyombo, ndiyo maana mimi nimeamua kusitisha maonyesho'', alisema Choki
Kiongozi wa Shoo wa bendi hiyo, Super Nyamwela (kulia) akiwaongoza wenzake kushambulia jukwaa katika onyesho la mwisho la bendi hiyo kabla ya kutimkia nchini Japan, hivi majuzi.

*********************************
Kabla ya kuondoka nchini Choki, aliitisha kikao cha dharula na kuwatangazia wanamuziki wake kuwa bendi hiyo imeamua kusitisha maonesho yake kwa muda, ambao haukutangazwa mwisho wake na kuwataka wasanii wote wanaounda bendi hiyo kufanya ustaarabu mwingine kwa kipindi hicho chote.

Baadhi ya wadau wa muziki nchini wamesema kuwa bendi hiyo haikuwa ikifanya vizuri na katika maonyesho yake ya hivi karibuni, huku Mkurugenzi wake Ally Choki, akionekana kutokuwa na mudi ya kufanya kazi na hasa tangu alipoondokewa na mke wake kipenzi mwaka jana.
Wanenguaji wa kike wa bendi hiyo, wakiwajibika jukwaani katika onyesho lao la mwisho kabla ya kuitishwa kikao cha kutangaziwa kufungwa kwa muda bendi hiyo.
******************************
''Inawezekana kifo cha mkewe ndiyo sababu kubwa ya kuyumba kwa bendi hiyo, na hasa kwa Choki ambaye muda mwingi alionekana kutokuwa na raha muda mwingi tangu alipofiwa na mkewe na hivyo kushindwa kufanya kazi kama alivyokuwa zamani ili kuwaridhisha mashabiki wake'', alisema mdau huyo wa muziki, aliyejitambulisha kwa jina la Kantoka kutoka Home Allone Kinondoni
Baadhi ya waimbaji wa bendi hiyo siku walipofanya onyesho lao la mwisho kabla ya Viongozi wao kuwatangazia kusimamisha maonesho ya bendi hiyo kwa muda usiojulikana.

No comments:

Post a Comment

SUFIANIMAFOTO Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.