Na Zainab Nyamka
MASHINDANO ya Johnnie Walker Waitara Trophy yanatarajiwa kuanza kutimua vumbi Januari 29 mwaka huu kwa zaidi ya wachezaji 100 kutoka katika klabu za Golf nchini kushiriki.
Akizungumza na waandishi wa habari leo, Mwenyekiti wa Klabu ya Gofu Lugalo,Brigedia Jenerali Mstaafu Michael Luwongo, amesema lengo la kuandaa mashindano hayo ni heshima ya kuendelea kimuenzi muasisi wa klabu hiyo,Jenerali George Waitara ambayo mashindano hufanyika kila mwaka mwezi Novemba lakini 2021 halikufanyika hivyo linafanyika mwaka huu.
Amesema kuwa mashindano hayo yatashirikisha wachezaji kutoka klabu zote za hapa nchini kama vile Moshi klabu, Arusha Gymkhana, Mufindi klabu,Morogoro Gymkhana,Dar es Salaam Gymkhana,Sea cliff golf klabu Zanzibar, Kili Golf na TPC Golf klabu.
Aliongeza kuwa mwaka huu mwitiko wa wachezaji ambao watakaoshiriki ni mkubwa kwa sababu Mpaka sasa wachezaji ambao wamesajiliwa kushiriki ni 100 na bado usajili unaendelea mpaka Alhamisi asubuhi ndio itakuwa mwisho wa kusajiliwa
"Maandalizi yanakwenda vizuri tuna uwezo wa kupokea idadi ya wachezaji wowote, watu waendelee kujisajili," amesema.
Aidha amesema nafasi ya watoto haitakuwepo kwa sababu ya wadhamini wao ni wa kileo hivyo ni kinyume na maadili na malezi ya watoto.
Kwa upande wake nahodha wa klabu hiyo, Meja Japhet Masai, amesema kuwa mashindano hayo ni ya siku moja ambapo wataanza na shindano la wachezaji wa kulipwa ambao watacheza siku ya Ijumaa na wachezaji wa ridhaa kwa maana ya Div A,B,C, Seniors,na Ladies watacheza siku ya Jumamosi Januari 29.
Naye Meneja Masoko wa Kampuni ya bia ya Serengeti, Lumuli Minga ambao ni wadhamini wa mashindano hayo, amesema ni jambo la furaha kwao kuendelea kutengeneza fursa mbalimbali katika michezo na wataendelea kujikita zaidi kwani michezo ni fursa na inatoa ajira kwa vijana.
"Katika hili shindano la Waitara Cup tupo kwa miaka mitatu na tutaendelea kuwa wadhamini, dhamira ni kuendeleza gofu nchini," amesema Lumuli
No comments:
Post a Comment