Habari za Punde

*WIZARA YA NISHATI NA MADINI YAZINDUA RASMI MFUMO WA KULIPIA LESENI ZA MADINI WA KIELETRONIKI

Na Jacquiline Mrisho- MAELEZO
Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini imezindua mfumo wa malipo ya ada za leseni za madini kwa njia ya mtandao ujulikanao kama Online Mining Cadastre Transactional Portal (OMCTP).
Akiongea na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam, Kamishna Msaidizi wa Madini anayeshughulikia leseni Bw. John Nayopa amesema kuwa mfumo huu wa kielektroniki unawawezesha wateja waliosajiliwa kutuma maombi ya leseni, kuhakiki taarifa za leseni wanazomiliki pamoja na kutuma taarifa za utendaji kazi kwa njia ya kielektroniki.
“Wizara ya Nishati na Madini imeanzisha mfumo huu kwa malengo ya kurahisisha upatikanaji wa taarifa za leseni, kuongeza kasi za utoaji wa leseni za madini, kupunguza tatizo la mlundikano wa maombi kwenye ofisi za madini na pia kurahisisha mawasiliano kati ya Wizara na wamiliki wa leseni,” alisema Nayopa
Aidha, Bw. Nayopa aliongeza kuwa mfumo huu wa kielektroniki unawawezesha wateja kupata ramani za kijiolojia na takwimu mbalimbali za madini pia inamrahisishia mteja kulipia ada za leseni kwa njia mbalimbali zikiwemo za mitandao ya simu, Maxmalipo, kadi za Benki pamoja na kuhamisha fedha kupitia Benki.
Pia Nayopa alizitaja nyaraka zinazohitajika ili kujisajili na mfumo huo wa kielektroniki kuwa ni pamoja na fomu za kuomba usajili ambazo zinapatikana kwenye tovuti za Wizara, leseni halisi pamoja na stakabadhi za malipo ya leseni husika.
Aidha, aliwataka wadau wengine ambao hawamiliki leseni wawasilishe fomu za usajili pamoja na hati za utambulisho na kuwataka wamiliki wanaowatuma mawakala kuwapa nguvu za uwakili (Power of Arttorney) ambazo zitawaruhusu mawakala hao kushughulikia leseni.
Nayopa amewataka wachimbaji wa madini nchini kujisajili kwenye ofisi za Madini ili kuendelea kutumia huduma za leseni kwa njia ya mtandao kwakuwa malipo ya ada za leseni yatafanyika kwa njia ya mtandao pekee.
Mpaka sasa Wizara ya Nishati na Madini imefanikiwa kusajili jumla ya leseni 8800 za madini nchini kwa kutumia mfumo huu wa kielektroniki ambapo idadi hiyo inajumuisha leseni za Kampuni, vikundi na watu binafsi.

No comments:

Post a Comment

SUFIANIMAFOTO Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.