Na Sufianimafoto Reporter, jijini
WANACHAMA wa klabu ya Yanga leo wamemuomba Mwenyekiti wa klabu hiyo, Lloyd Nchunga, kuitisha Mkutano mkuu ili kuwajadili wanachama wanaochochea vurugu ndani ya Klabu hiyo kwa ajili ya kupata muafaka pamoja na kutaka mchanganuo wa mapato na matumizi ndani ya klabu hiyo tangu uongozi wa aliyekuwa Mwenyekiti wao aliyepita, Imani Madega.
Mkutano huo uliofanyika katika tawi la Buguruni leo mchana, jumla ya viongozi wa matawi 26 wameweza kuhudhuria na kutoa dukuduku za matatizo yao huku wakilaani vitendo vya baadhi ya wanachama wa klabu hiyo kutoa maneno ya kejeli kwa mdhamini wa Yusuph Manji wanaozungumza kwenye vyombo vya habari bila utaratibu kumtaka ajiondoe pamoja na baadhi ya viongozi waliopo madarakani.
Mratibu wa mkutano huo, Bakili Makele, alisema katika mkutano huo iwapo utaitishwa na Mwenyekiti wao, lengo ni kujadili mapato na matumizi ya klabu pamoja na kumaliza mgogoro uliofumuka ndani ya klabu hiyo.
"Kumekuwapo na vitendo vinavyorudisha nyuma maendeleo ya klabu na kusababisha timu ifanye vibaya katika michezo yake hali inayofanya kuwepo na mpasuko ndani ya Yanga,
"Kikubwa tunataka ufanyike mkutano ili tutoe madukuduku yetu, hali si nzuri kabisa kama mnavyoona, timu haifanyi vizuri, wanachama wamegawanyika kuna ambao wanatumiwa na baadhi ya viongozi ili kutuvuruga, sasa ni bora ijulikane moja na pia tupate mchanganuo mzima wa mapato na matumizi," alisema Makere.
Naye Mwenyekiti wa matawi kanda ya Ilala, Amir Ally alisema kufanyika kwa mkutano huo kutaleta amani kwani yote yatajulikana hapo na timu kuweza kufanya vizuri.Mwenyekiti wa klabu hiyo, Lloyd Nchunga alisema kuwa bado wanafanyia kazi maombi hayo japo kimsingi wamekubaliana na wanachama hao.“Tarehe rasmi ya mkutano itajulikana hapo baadaye, tunasubiri taarifa maalum ya kimaandishi,” alisema Nchunga.
No comments:
Post a Comment