Habari za Punde

*NIMR YAENDELELEA KUWA KINARA TAFITI ZA MAGONJWA YA BINADAMU

Mtafiti toka Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu  NIMR kituo cha Muhimbili Dkt. Godfather Kimaro akitoa wito kwa wanchi kujitokeza kwa aajili ya kupima afya zao mara tu wanapoona dalili za ugonjwa wa Kifua Kikuu ili kupunguza maambukizi mapya. Katikati ni Mkurugenzi wa NIMR kituo cha Muhimbili Dkt Godfrey Mfinanga na wa mwisho kulia ni Afisa habari Idara ya Habari MAELEZO Frank Mvungi.
************************************************
Frank Mvungi-Maelezo
Serikali yaendelea kuimarisha Tafiti za kifua kikuu hapa nchini  kwa kushirikiana na Taasisi za Kimataifa.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa  ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) kituo cha Muhimbili Dkt.Godfrey Mfinanga wakati wa mkutano na waandishi wa Habari leo jijini Dar es salaam.

Akieleza Dkt.Mfinanga alisema kuwa NIMR kituo cha Muhimbili imefanikiwa kwa kiasi kikubwa katika tafiti kwa kushirikiana na Taasisi za kimataifa kama African Research Consortium for Ecosystem and Population Health (AFRIQUE ONE CONSORTIUM) na East African Consortium for Clinical Research ( EACCR).
Dkt Mfinanga alibainisha kuwa wastani  wa wagonjwa 295 kati ya watu 100,000  hugundulika kuwa na TB ,ambapo Tanzania bara ilionekana kuwa na wagonjwa wengi zaidi kuliko Tanzania Visiwani,Vijijini kuliko mijini,watu wazima kuliko vijana,ambapo utafiti huo uko hatua za mwisho.

Akifafanua zaidi amesema tafiti zimeonyesha kuwa kwa wastani wa asilimia 35 ya wagonjwa wa TB huchelewa kugundulika  kutokana na uelewa mdogo na tabia ya wananchi walio wengi kuchelewa kwenda Hosipitali.
Dkt Mfinanga  alitaja maeneo yanayoathiriwa na Ugonjwa wa kifua kikuu kuwa ni mapafu ,tezi,tumbo,figo, na hata ubongo ikiwa mgonjwa hatapata matibabu kwa wakati muafaka.
Katika hatua nyingine Dkt Mfinanga amesema kuwa  NIMR kituo cha Muhimbili imefanya utafiti ambao umethibitisha kuwa kuna umuhimu  wa kushirikisha jamii katika kusimamia matibabu ya wagonjwa wa TB (Community DOT-PCT).
Kufuatia utafiti huo Serikali ilianzisha mfumo huo ambao umeonyesha mafanikio makubwa kwa kuwa mgonjwa anachagua mahali pa kumezea dawa za TB kati ya nyumbani akisimamiwa na ndugu au kwenye kituo cha tiba akisimamiwa na mtoa huduma wa afya.
Naye mtafiti toka NIMR kituo cha Muhimbili Dkt. Godfather  Kimaro alitoa wito kwa wananchi kuwahi hosipitali pale wanapoona dalili za ugonjwa wa Tb ambazo baadhi yake ni kikohozi kwa muda wa wiki mbili,homa za mara kwa mara na kukonda.
Kituo cha Utafiti cha Muhimbili (NIMR  Muhimbili Centre) ni moja ya vituo nane vya Taasisi ya utafiti wa magonjwa ya Binadamu (NIMR) Kituo cha Muhimbili kilirithiwa kutoka lililokuwa Baraza la Afrika ya Mashariki mwaka 1980 wakati Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa magonjwa ya Binadamu ilipoanzaishwa kwa sheria ya Bunge Namba 23 ya mwaka 1979.

No comments:

Post a Comment

SUFIANIMAFOTO Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.